Saturday, December 09, 2017

BOSI WA NDEMLA ASHINDWA KUTUA BONGO KUMALIZANA NA SIMBA

BOSI wa Klabu ya AFC Eskelistuna ameshindwa kuwasili nchini wiki hii kumalizana na Simba kuhusu usajili wa timu hiyo, Said Ndemla baada ya mmoja kati anayehusika na ujio wake kupata msiba.

Kiongozi huyo alitarajiwa kuwasili nchini wiki hii kwa ajili ya suala la mchezaji huyo pamoja na masuala mengine ya kisoka lakini imeshindikana.

Ndemla alifanikiwa kufuzu majaribio mwezi uliopita katika klabu hiyo ya Sweden ambayo ilikuwa
 inashiriki ligi kuu na sasa imeshuka daraja.

Akizungumza na Championi Jumamosi, meneja wa Ndemla, Jamali Kisongo alisema kiongozi huyo ameshindwa kuwasili kutokana na matatizo hayo aliyoyapata mwenzao.

“Yule kiongozi alitakiwa kuwasili nchini wiki hii lakini imeshindikana kwa sababu mmoja kati ya watu anayehusika na ujio wake amepata msiba, hivyo sijafahamu baada ya hapo ratiba zake zitakuwaje.

“Lakini kama kutakuwa na lolote tutaweka wazi. Kwa upande wa mchezaji licha ya timu kushuka daraja lakini dili liko palepale, atajiunga nayo tu,” alisema Kisongo.